Ticker

6/recent/ticker-posts

MAKALLA ARIDHISHWA NA UPATIKANAJI HUDUMA YA MAJI KIBAMBA



Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Amos Makalla ameridhishwa na hali ya upatikanaji wa maji katika jimbo la Kibamba baada ya ziara ya mtaa kwa mtaa kwenye Kata ya Kwembe na Kibwegere na kujionea upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi baada ya kuwepo changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa maji.

Mhe. Makalla amesema lengo la ziara hii ni utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan la kufuatilia na kujiridhisha hali ya upatikanaji wa huduma ya maji kwa wanaoishi pembezoni ya miji.

"Nipo hapa kutekeleza agizo la Mhe. Rais Mama Samia Suluhu la kupita, kukagua na kuona ni kwa namna gani wananchi wanapata huduma ya maji. Nimeridhishwa na hali niliyoikuta niwapongeze DAWASA kwa kazi nzuri vile mnavyotuandikia kwenye ripoti ndio vitu tunaviona vimetekelezeka hakikisheni huduma inakua endelevu na kila mwananchi aliyeomba huduma anaipata." amesema Mhe. Makalla.

Akitoa taarifa fupi ya upatikanaji huduma kwa eneo la Kibamba, Meneja wa Mkoa wa Kihuduma DAWASA-Kibamba Ndugu Elizabeth Sankere amesema ndani ya Kata ya Kwembe na Kibwegere changamoto ya ukosefu wa huduma ya maji kwa ilichangiwa na sababu za kijiographia ya eneo na vilevile ongezeko la watu ambapo ilipelekea miundombinu kuzidiwa na kutokidhi mahitaji ya wananchi huku akibainisha kwa sasa huduma inapatikana kwa asilimia 90 baada ya jitihada zilizofanywa na Serikali kupitia DAWASA ambapo miradi imefanyika na inaendelea kufanyika kwa maeneo yaliyobaki kupata huduma.

"Kwa upande wa ofisi ya DAWASA Kibamba tunahudumia kata tano zenye wateja 25,000 na hali ya upatikanaji maji kwenye kata hizo ni asilimia 90. Tumefanikiwa kuwa na mtandao wa mabomba wa zaidi ya kilomita 200,000 kwa eneo lote tunalolihudumia"aliongeza

"Kwa maeneo yaliyokuwa na changamoto hapo awali, Mamlaka ilipeleka miradi ya kuongeza mtandao wa maji na jitihada zinaendelea kwa maeneo yaliyobaki" amesema Ndugu Elizabeth

Naye, Ndugu Joyce Kijumbe Mkazi wa Mji mpya Kwembe ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuwaondolea adha ya maji iliyokuwepo katika mtaa wao kwa mda mrefu hali ilyowapelekea kuingia gharama kubwa kupata huduma ya maji

"Kwa kweli tunamshukuru Mhe. Rais Mhe. Samia Suluhu ametuheshimisha sisi wanawake tumepitia shida kubwa lakini sasa tunafuraha maji yapo, tunafanya kazi zetu kwa raha na gharama imepungua pia" ameeleza Ndugu Joyce

Post a Comment

0 Comments