Ticker

6/recent/ticker-posts

TCCIA YAIOMBA SERIKALI KUBORESHA MIUNDOMBINU VIWANJA VYA MAONESHO TANGA.

Na Hamida Kamchalla, TANGA.

MIUNDOMBINU mibovu ya barabara katika viwanja vya maonesho ya biashara na utalii vilivyopo eneo la Mwahako jijini Tanga hasa katika kipindi hiki cha mvua yamepelekea Chemba ya Biashara Mkoa wa Tanga (TCCIA) kuiomba serikali ya jiji na Mkoa kufanya maboresho ya mara kwa mara pindi ifikapo muda wa maonesho hayo.
Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Rais wa TCCIA ( VIWANDA) Vicent Minja wakati wa uzinduzi wa maonesho ya 10 ya biashara na utalii katika viwanja hivyo ambapo pia alimuomba mkuu wa Mkoa wa Tanga Waziri Kindamba kutoa tamko kuhusu mpangilio wa maeneo halo yakiwemo na ya wafanyabiashara wadogo (machinga).


"Tuna kero ya uwanja, kama tunavyoona hapa leo mvua imenyesha, napenda kushauri uongozi wa Mkoa na jiji, tuweze kushirikiana na sekta binafsi, haya maonesho siyo ya TCCIA pekee bali ni Tanga nzima ambayo yanajenga uwezo wa Mkoa kuweza kupata watu watakaonunua bidhaa za Tanga na kuendeleza Mkoa wao" amesema.


"Kwahiyo tunapotoa maamuzi yanayohusiana na hili tuone kabisa tunatoa mahusiano ya Mkoa na siyo ya TCCIA, hivyo niombe uongozi wa Mkoa tuone namna sahihi, nzuri yenye miundombinu ambayo itayafanya haya maonesho yawe ya Kimataifa" amesema Minja.


Aidha Minja amefafanua kwamba endapo miundombinu itaboreshwa na wageni kutoka nje ya nchi kukaribishwa kuja na kununua bidhaa itapelekea pia kuweza kuwavuta wawekezaji kuja na kuwekeza katika maeneo ya viwanda na mengineyo.


"Kwahiyo hili naliacha kwa wenzetu wa sekta ya Umma waangalie na kuiga mafanikio ya Mikoa mingine, wajenge mabanda ya kudumu kama vile Bandari na sekta nyingne kubwa ili pia watu wanaweza kukutana na kushirikiana katika mambo muhimu" amesema.


Mbali na hayo Minja pia ameiomba ofisi ya mkuu wa Mkoa kutoa mwongozo wa uboreshaji wa maeneo likiwemo la wafanyabiashara ndogondogo (machinga) ambapo kwa sasa wanauza bidhaa zao maeneo ambayo yanaonekana siyo rasmi.


Hata hivyo wadau wa maonesho hayo wameelea kwamba muitikio siyo mkubwa kama walivyotazamia baada ya maonesho ya mwaka uliopita 2022 kwamaana washiriki walikuwa wengi na baadhi walitokea nje ya Mkoa wa Tanga, hivyo walitegemea mwaka huu yangekuwa makubwa na ya kufana zaidi.


Mbali na hayo wamekumbwa na wasiwasi kutokana na maji kujaa ndani ya baadhi ya mabanda kutokana na miundombinu kutokuwa ya uhakika hali inayoashiria wananchi kutokuwa wengi kwenye maonesho hayo kwakuwa hata barabara hazipitiki kwa uhuru kutokana na kujaa maji.


Baadhi ya wananchi wanaofika katika maonesho hayo wamesema hali ya mvua itasababisha watu wengi kukaa majumbani mwao kwani barabara hazipitiki kwa wakati lakini pia wapo watoto ambao wanahitaji kwenda kuangalia wanyama laying wanashindwa kutokana na hali hiyo.


"Mwaka huu hali imekuwa tofauti kabisa na mwaka jana, siku kama ya leo nakumbuka hapa palifurika watu wanaoibgia mbali na wanaotoka, hata kupishana ilikuwa ni shida, laminitis sasa his mvua imefanya watu wengi wasije, hatujajua siku ya mwisho itakuaje laminitis kama hali itaendelea hivi basi safari hii ni kama yamebuna" alisema Mwanahamisi mkazi wa Mwang'ombe.
Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Conrad Milinga alipotembelea banda la Bodi ya Mkonge.
Banda la TANAPA, Ofisa Muhifadhi wa Bodi ya Utalii, Willy Halule akitoa elimu kwa mteja wake.
Kaimu Conrad Milinga akipokea zawadi alipotembelea banda la TANAPA
Kaimu Conrad Milinga akikagua banda la Sisalana.

Post a Comment

0 Comments