Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI IMEWAGIZA WAKUU WA TAASISI ZA UMMA KUWEKA UTARATIBU WA KUFANYA MAZOEZI


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwapungia mikono wachezaji Oktoba 23, 2021 wakati wa maandano ya ufunguzi wa Mashindano ya Michezo ya Wizara na Idara za Serikali Tanzania (SHIMIWI) yanayoendelea mjini Morogoro.

Baadhi ya watumishi wakipita mbele ya Mgeni Rasmi ambaye ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango wachezaji leo Oktoba 23, 2021 wakati wa maandano ya ufunguzi wa Mashindano ya Michezo ya Wizara na Idara za Serikali Tanzania (SHIMIWI) yanayoendelea mjini Morogoro.

************************

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ameziagiza Wizara, Idara, Wakala za Serikali, Taasisi pamoja na Sekretarieti za Mikoa kuweka utaratibu wa kufanya mazoezi kwa watumishi wote walau mara moja kwa wiki ili kuimarisha afya zao hatua inayosaidia kuleta tija katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Mpango amesema hayo leo Oktoba 23, 2021 mkoani Morogoro alipokuwa akifungua rasmi Mashindano ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayoendelea mkoani humo.

“Ninawaagiza Watendaji wakuu wote wa Wizara, Idara, Wakala za Serikali, Taasisi za Serikali na mikoa yote mhakikishe mnapanga mapema na kutenga bajeti ya masuala ya michezo na muwaruhusu watumishi wafanye mazoezi mapema ili kujiandaa vyema na mashindano ya SHIMIWI” amesema Makamu wa Rais Mhe. Dkt. Mpango.

Ili kuyafanya mashindano haya kuwa bora zaidi, Dkt. Mpango ameiagiza Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo kupitia Michezo na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kuendelea kusimamia kanuni za uongozi bora kwa kushirikiana na vyama vya michezo nchini.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Sanaa, Utamaduni na Michezo Dkt. Hassan Abbasi amewahimiza waajiri wawaruhusu watumishi kushiriki mashindano ya SHIMIWI kwa kuzingatia michezo ni jambo la kimkakati katika taifa ikiwa ni nguvu laini ya nchi duniani kote.

Katibu Mkuu Dkt. Abbasi ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapenda na kuwajali watumishi na inajali na kupenda michezo.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri mwenye dhamana ya michezo Dkt. Abbasi amemshukuru Mhe. Makamu Rais kwa kukubali kuwa mgeni rasmi na kuja kufungua mashindano hayo kwa niaba ya Mhe. Rais na amemhakikishia kuwa Wizara yake ipo mstari wa mbele katika kusimamia mageuzi makubwa ya michezo nchini ambapo mafaniko yake yameanza kuonekana katika timu za taifa zinazoliwakilisha nchi yetu katika michezo mbalimbali kimataifa katika kipindi kifupi cha Serikali ya Awamu ya Sita.

Miongoni mwa mafanikio hayo ni hadi sasa timu ya Taifa ya wanaume inaongoza kwenye kundi lao katika hatua za kufuzu kucheza kombe la dunia mwakani, timu ya Taifa ya Wanawake Twiga Stars ni bingwa wa mashindanio ya COSAFA 2021, Timu ya taifa ya Kriketi ni mabingwa kwa nafasi ya tatu Afrika, timu ya Kriketi ya U-20 waliocheza nchni Rwanda imeshika nafasi ya tatu Afrika.

Post a Comment

0 Comments