Ticker

6/recent/ticker-posts

DC TANDAHIMBA AIPONGEZA REA

Kazi ya kusimika nguzo za umeme ikiendelea katika kijiji cha Mtua, wilayani Nachingwea, Mkoa wa Lindi wakati wa ziara ya Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo (mwenye fulana ya mistari) na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (fulana ya njano), Novemba 24, 2021.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala (kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy Kitabu kinachoelezea utamaduni wa eneo hilo. Mhandisi Saidy alimtembelea Mkuu wa Wilaya akiwa katika ziara ya kazi, Novemba 24, 2021.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala (kushoto) akimkabidhi Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo, Kitabu kinachoelezea utamaduni wa eneo hilo. Wakili Kalolo alimtembelea Mkuu wa Wilaya akiwa katika ziara ya kazi, Novemba 24, 2021.
Kazi ya kusimika nguzo za umeme ikiendelea katika kijiji cha Mtua, wilayani Nachingwea, Mkoa wa Lindi. Taswira hii ilichukuliwa wakati wa ziara ya Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (hawapo pichani), Novemba 24, 2021.
Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo (wa pili-kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (wa tatu-kushoto), wakikagua shimo lililoandaliwa kwa ajili ya kusimika nguzo ya umeme katika kijiji cha Mtunungu, wilayani Masasi, Mkoa wa Mtwara. Viongozi hao wa REA walikuwa katika ziara ya kazi Novemba 24, 2021.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala (kulia) akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Wakili Julius Kalolo, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy pamoja na watalaam kutoka REA na TANESCO. Viongozi hao wa REA walikuwa katika ziara ya kazi Novemba 24, 2021.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mtwara, Yusuf Nannila (katikati), akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo (kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (kushoto). Viongozi hao wa REA walikuwa katika ziara ya kazi Novemba 24, 2021.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala (katikati) akionesha vijiji vya wilaya hiyo vilivyofikiwa na umeme na ambavyo havijafikiwa kwa kutumia ramani ya mkoa wa Mtwara kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Wakili Julius Kalolo (kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kushoto). Viongozi hao wa REA walikuwa katika ziara ya kazi Novemba 24, 2021.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy (hawapo pichani). Viongozi hao wa REA walimtembelea Mkuu wa Wilaya ofisini kwake, Novemba 24, 2021 wakiwa katika ziara ya kazi.
Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo (wa tatu-kushoto), Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (wa tatu-kulia) na wataalam kutoka REA na TANESCO, Novemba 24, 2021. Ujumbe wa REA ulikuwa katika ziara ya kazi.

***********************************
Na Veronica Simba, REA - Mtwara

Mkuu wa Wilaya ya Tandahimba, Kanali Patrick Sawala ametoa pongezi kwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kutokana na kazi nzuri inayofanyika kupeleka umeme vijijini.

Alitoa pongezi hizo ofisini kwake wakati akizungumza na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Wakili Julius Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, waliokuwa katika ziara ya kazi, Novemba 24, 2021.

“Tunawapongeza na kuwashukuru REA kwa kushirikiana na TANESCO. Tunatambua kazi kubwa mnayoifanya na tunafarijika sana,” alisema Kanali Sawala.

Aidha, Mkuu wa Wilaya alipongeza kasi ambayo REA imeanza nayo katika kutekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili wilayani humo na kusisitiza kuwa iendelee hivyo ili vijiji vilivyosalia vipate umeme kwa wakati uliopangwa.

Vilevile, alipongeza maelekezo yaliyotolewa na Uongozi wa REA kwa mkandarasi anayetekeleza miradi ya umeme vijijini wilayani humo, kuandaa Mpango Kazi na kuuwasilisha katika ofisi yake, ofisi ya mbunge, diwani na serikali za mitaa akisema kuwa itarahisisha ufuatiliaji wa utendaji kazi hatua kwa hatua.

Akifafanua zaidi, Kanali Sawala alisema kuwa wananchi wanapaswa kufahamu kinachofanyika, namna watakavyonufaika na mradi husika na kwa wakati gani kwani kwa namna hiyo watatoa ushirikiano mzuri katika utekelezaji wake.

Pia, alitoa rai kwa Wakala kutekeleza kwa haraka kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya wilaya hiyo vilivyoko mpakani mwa nchi ili kuwezesha uimarishaji zaidi wa ulinzi na usalama wa nchi.

Katika hatua nyingine, viongozi hao wa REA walimtembelea Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mtwara, Yusuf Nannila na kuzungumza naye kuhusu utekelezaji wa Ilani ya CCM hususan katika sekta ya nishati vijijini.

Mwenyekiti huyo wa CCM alieleza kuwa Uongozi wa Chama unafarijika kuona maelekezo yaliyotolewa katika Ilani kuhusu sekta ya nishati vijijini, yanatekelezwa kwa vitendo.

“Leo tunashuhudia kwamba Ilani yetu haikuwa maneno matupu bali ni matendo kama inavyojidhihirisha sasa,” alisema.

Hata hivyo, Nannila alitoa wito kwa watendaji wa serikali kuendelea kuchapa kazi kwa bidii ili vijiji vyote vifikiwe na umeme ifikapo mwishoni mwa mwezi Desemba, 2022 kama ilivyoelekezwa katika Ilani ya CCM.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mwenyekiti wa Bodi, Wakili Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Saidy, walimhakikishia Mkuu wa Wilaya na Mwenyekiti wa CCM kuwa watatekeleza maagizo yote waliyowapatia.

Walieleza kuwa REA imejipanga kuhakikisha inatekeleza azma ya serikali kufikisha umeme katika vijiji vyote ifikapo mwishoni mwa Desemba, 2022.

Aidha, walieleza kuwa Wakandarasi wote wanaotekeleza miradi ya umeme vijijini nchini, wameshajulishwa kuwa hakutakuwa na ongezeko la muda wa kukamilisha miradi hiyo, hivyo wanapaswa wajipange kuhakikisha miradi inakamilika kwa muda uliopangwa.

Wakili Kalolo alimwomba Mwenyekiti wa CCM kufikisha salamu za shukrani kutoka REA kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kutokana na kuendelea kuwezesha utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini na kwamba REA inaahidi haitamwangusha.

Akifafanua zaidi kuhusu utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili mkoani Mtwara, Mhandisi Saidy alieleza kuwa umelenga kuvifikishia umeme vijiji 402 vilivyosalia.

Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Wakili Julius Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy wako katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini katika mikoa ya Ruvuma, Mtwara, Lindi na Pwani.

Post a Comment

0 Comments