Ticker

6/recent/ticker-posts

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI KASEKENYA AWAPONGEZA TANRODS SINGIDA UJENZI WA DARAJA LA MSINGI

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya (katikati) akizungumza na wataalamu wakati akikagua Daraja la Msingi lenye thamani ya Sh.Bilioni 10.9 linalojengwa wilayani Mkalama mkoani Singida wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja aliyoifanya hivi karibuni.
Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Singida Mhandisi Matari Masige (kulia) akimuelekeza jambo Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya
Mafundi wa Kampuni ya Kizawa ya Gemen Engineering Ltd inayojenga daraja hilo wakiendelea na kazi.
Mafundi wa Kampuni ya Kizawa ya Gemen Engineering Ltd inayojenga daraja hilo wakimsikiliza Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya (hayupo pichani) wakati wa ziara hiyo.

**************************
Na Dotto Mwaibale, Singida


NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mhandisi Godfrey Kasekenya amewapongeza Wakala wa Barabara Tanzania (TANR0DS) Mkoa wa Singida kwa kazi nzuri ya ujenzi wa daraja la Msingi lililopo wilayani Mkalama mkoani hapa.


Kasekenya alitoa pongezi hizo hivi karibu katika ziara yake ya kikazi ya siku moja ya kukagua ujenzi wa daraja hilo ambalo ni muhimu sana kiuchumi kwa wananchi wa mikoa ya Simiyu, Singida na mingibmne jirani watakao litumia.


Waziri Kasekenya alisema hakuna miradi inayofanywa na Serikali itakayo simama na kuwa daraja hilo limeainishwa kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na lipo kwenye mpango wa wizara wa kati ya madaraja makubwa yanayojengwa yanayotarajiwa kukamilishwa ni pamoja na hilo.


Alisema maendeleo ya ujenzi wa daraja hilo ni mategemeo makubwa ya Serikali kuona linakamilika kwa wakati na wananchi wanalitumia.


Alisema nia ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuona wakandarasi wazawa wenye sifa wanapewa kazi ili watoe ajira ikiwemo kukuza uchumi wa nchi.


Alimtaka mkandarasi mzawa Gemen Engineering Company Ltd anaye jenga daraja hilo na Mhandisi Mshauri kukamilisha ujenzi huo Mwezi Juni mwakani na hata kabla ya mwezi huo ili kujijengea heshima.

"Ili kujiheshimisha kamilisheni ujenzi huu kwa wakati na kwa viwango vya juu na si vinginevyo" alisema Kasekenya.


Awali akitoa taarifa ya ujenzi huo Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Singida Mhandisi Matari Masige alisema mradi huo unaojengwa na Mkandarasi Mzawa Gemen una thamani ya Sh.10.9 Bilioni na kuwa umefikia asilimia 75.5.


Alisema kiasi cha fedha alicholipwa mkandarasi ni Sh.5.5 Bilioni sawa na asilimia 50 na kuwa hela iliyosaliwa kulipwa ni Sh. 1.7 Bilioni.

Post a Comment

0 Comments