Ticker

6/recent/ticker-posts

ELIMU YA FEDHA KUFUNGUA FURSA ZA UWEKEZAJI


Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Charles Mwamwaja, akizungumza na waandishi wa habari ambapo aliwakaribisha wananchi kuhudhuria maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam yatakayofanyika kwa siku 7.


Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Charles Mwamwaja, akizungumza na waandishi wa habari ambapo alitoa wito kwa wananchi kufika katika maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam yatakayofanyika kwa siku 7 ili kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo masuala ya mikopo na riba zake.


Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Charles Mwamwaja akizungumza na Bi. Mwanahamisi Mketo mmoja wa wajasiliamali kutoka kikundi cha Uwazi Makangarawe waliowezeshwa na TASAF alipotembelea mabanda mbalimbali yaliyoshiriki maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.


Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Charles Mwamwaja akipokelewa na Kamishana Msaidizi wa Idara hiyo Bi. Dionisia Mjema alipowasili kwenye maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.


Afisa Tehama kutoka Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Emmanuel Maendaenda akitoa maelezo kwa Bw. Jafet Mzava alipotembelea banda la wizara hiyo kwenye maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.


Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Benny Mwaipaja, akimwongoza Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Charles Mwamwaja (katikati), kutembelea mabanda ya walioshiriki maonesho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam. Kulia ni Kamishana Msaidizi wa Idara hiyo Bi. Deoninsia Mjema.

(Picha na WFM)

*********************************

Na. Peter Haule na Josephine Majura, WFM, Dar es Salaam

Kamishna wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha nchini, Dkt. Charles Mwamwaja amesema kuwa watanzania chini ya asilimia 50 ndio waliofikiwa na huduma za fedha jambo ambalo limeifanya Serikali kuwa na Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa ili kuongeza uelewa kwa wananchi kwa lengo la kuchochea ustawi wa jamii.

Hayo ameyabainisha wakati akitembelea mabanda katika maonesho ya Wiki ya Fedha yanayoendelea katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam ikiwa ni siku ya kwanza ya maonesho hayo.

Alisema huduma za fedha zinarahisisha utaratibu wa kubadilishana bidhaa na huduma jambo ambalo ni muhimu katika maendeleo ya uchumi kwa nchi yeyote Duniani ikiwemo Tanzania hivyo ni lazima kuwa na mkakati wa kutoa elimu kwa umma kuhusu uelewa wa huduma hiyo.

“Watu wanadhulumiwa na hawajui waende wapi, nani ni mtoaji wa huduma hiyo rasmi, mteja akidhulumiwa aende wapi na hawajui kuwa mteja wa huduma za fedha analindwa, hivyo Serikali imeamua kutoa elimu kwa umma ili kuondoa sintofahamu hiyo”. alieleza Dkt. Mwamwaja

Dkt. Mwamwaja alisema kuwa Sekta ya Fedha inarahisisha upatikanaji wa mitaji na uwekezaji ndio maana vikundi vidogo vya kuweka na kukopa kama Vikoba, vinasaidia kukuza mitaji ambayo inaweza kutumika kuwekeza kwenye miradi ya ufugaji na mingine ambayo inamanufaa si tu kwa mtu mmoja mmoja bali kwa Taifa kwa ujumla.

Aidha alisema matokeo chanya ya Sekta ya Fedha hayawezi kufikiwa bila kuwekeza katika elimu ili wananchi waweze kutumia fursa zilizopo kwa maendeleo yao na nchi kwa ujumla.

Vilevile Dkt. Mwamwaja alisema umbo la Sekta ya Fedha limegawanyika katika maeneo matano ambayo ni masuala yanayohusiana na huduma za Benki, Bima, Masoko ya Mitaji na Dhamana, Mifuko ya Jamii na Huduma ndogo ya Fedha.

Maonesho ya Huduma za Fedha Kitaifa yameanza Novemba 8 na kutarajiwa kuhitimishwa Novemba 14 mwaka huu katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam.

Post a Comment

0 Comments