Ticker

6/recent/ticker-posts

MKUU WA MKOA WA LINDI AHIMIZA ULIPAJI KODI WA HIARI KWA AJILI YA KULETA MAENDELEO NCHINI

Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainab Telack akizungumza na ujumbe kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ukiongozwa na Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Msafiri Mbibo 25/11/2021 wakati wa ziara ya kikazi mkoani hapo yenye lengo la kuoata taarifa kuhusu utendaji kazi na tathmini ya maadili katika ukusanyaji wa kodi na utoaji wa huduma za TRA mkoani hapo.


Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainab Telack (kulia) akizungumza na Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Msafiri Mbibo 25/11/2021 wakati wa ziara ya kikazi mkoani hapo yenye lengo la kuoata taarifa kuhusu utendaji kazi na tathmini ya maadili katika ukusanyaji wa kodi na utoaji wa huduma za TRA mkoani hapo.


************************************

Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Zainab Telack akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ukiongozwa na Naibu Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Msafiri Mbibo 25/11/2021 wakati wa ziara ya kikazi mkoani hapo yenye lengo la kuoata taarifa kuhusu utendaji kazi na tathmini ya maadili katika ukusanyaji wa kodi na utoaji wa huduma za TRA mkoani hapo.

MKUU wa Mkoa wa LINDI, Mhe. Zainab Telack amewataka Wakazi mkoani hapo kuchangamkia fursa ya kufungua biashara mbalimbali ili waweze kuisadia Serikali katika kuendeleza maendeleo kwa kulipa kodi kwa hiari na kuwataka wafanyabiashara kuhakikisha kwamba wanatoa risiti halali za EFD na wananchi kudai risiti kwa kila manunuzi au huduma wanazopewa.

Kauli hiyo ameitoa leo ofisini kwake wakati alipokutana na Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bwana Msafiri Mbibo ambaye yupo katika ziara ya kikazi mkoani hapo kwa ajili ya kutembelea ofisi za TRA kujionea utendaji kazi na kupokea taarifa ya tathmini ya maadili katika ukusanyaji wa kodi na utoaji huduma.

“Kodi tunazolipa ndiyo zinakwenda kuimarisha uchumi wa nchi yetu, lakini ndiyo zinakwenda kujenga miundombinu mbalimbali ndani ya nchi yetu kama vile ujenzi wa barabara, vituo vya afya na vitu vingine vingi, hivyo nitoe wito kwa Watanzania wenye uwezo wa kufanya biashara wafungue biashara ili waweze kuisaidia Serikali katika kukuza maendeleo nchini”, alisema Telack.

Ameongeza kuwa, tangu Serikali ya Awamu ya Sita iingie madarakani, tayari imefanya maendeleo mbalimbali makubwa na hadi sasa tayari mkoa huo umeshapokea zaidi ya shilingi bilioni 35 kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo mkoani hapo.

Kwa upande wake Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bwana Msafiri Mbibo amesema kwamba lengo la ziara yake mkoani hapo ni kukutana na watumishi wa TRA mkoani Lindi ikiwemo kukutana na Jumuiya ya Wafanyabiashara mkoani hapo na kujadiliana masuala mbalimbai yanayohusu kodi ikiwemo kusikiliza kero zao na kuzitatua.

Ameongeza kuwa, TRA inalenga kukutana mara kwa mara na wafanyabiashara, kusikiliza changamoto zao na kutafuta namna ya kuzitatua ili wasikwame katika shughuli zao za kibiashara lakini pia inakutana na watumishi ili kuwajengea uwezo katika kuwahudumia vema walipakodi wote.

“Tunasisitiza uhusiano mzuri kati ya TRA na jamii ya walipakodi ya Mkoa wa Lindi na nchini kote ili uweze kuimarika na sisi tutaendelea kuongea na watumishi na jumuiya za wafanyabiashara ili kufahamishana mambo mbalimbali ya kiutendaji na ulipaji kodi kwa ujumla”, alisema Mbibo.

Naibu Kamishna Mkuu wa TRA yupo ziarani katika mikoa ya Kusini mwa Tanzania ya Lindi, Mtwara na Ruvuma kwa lengo la kutembelea ofisi za TRA na kupokea taarifa ya tathmini ya maadili katika ulipaji wa kodi na utoaji huduma kwa ujumla.

Post a Comment

0 Comments