Ticker

6/recent/ticker-posts

DC CHEMBA NA BABATI MJINI WAIPONGEZA TBS KWA KUTOA MAFUNZO KUHUSU UDHIBITI SUMUKUVU KWA MAZAO


Mkuu wa Wilaya ya Chemba,Simon Chacha akizungumza wakati wa mafunzo kuhusu Udhibiti wa Sumukuvu kwa mazao ya Mahindi,karanga kwa wafanyabiashara,wasafirishaji na wasindikaji kutoka katika Wilaya ya Chemba yaliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia Mradi wa Kudhibiti Sumukuvu Tanzania- TANIPAC.


Sehemu ya washiriki wakifatilia hotuba ya kuu wa Wilaya ya Chemba,Simon Chacha ,wakati wa mafunzo kuhusu Udhibiti wa Sumukuvu kwa mazao ya Mahindi,karanga kwa wafanyabiashara,wasafirishaji na wasindikaji kutoka katika Wilaya ya Chemba yaliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia Mradi wa Kudhibiti Sumukuvu Tanzania- TANIPAC.


Mkuu wa Wilaya ya Chemba,Simon Chacha akiwa katika picha ya pamoja na washiriki mara baada ya kufungua mafunzo kuhusu Udhibiti wa Sumukuvu kwa mazao ya Mahindi,karanga kwa wafanyabiashara,wasafirishaji na wasindikaji kutoka katika Wilaya ya Chemba yaliyoandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia Mradi wa Kudhibiti Sumukuvu Tanzania- TANIPAC.

..........................................

Na Alex Sonna-CHEMBA NA BABATI

WAKUU wa Wilaya za Chemba na Babati Mjini wamewataka wafanyabiashara,wasafirishaji na wasindikaji wa vyakula kuzingatia mikakati ya kukabiliana na changamoto ya sumukuvu ili vyakula viendelee kuwa salama kwa muda wote.

Kauli hizo wamezitoa kwa tofauti wakati wakifungua mafunzo kuhusu Udhibiti wa Sumukuvu kwa mazao ya Mahindi,karanga kwa wafanyabiashara,wasafirishaji na wasindikaji kutoka katika Wilaya ya Chemba.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kupitia Mradi wa Kudhibiti Sumukuvu Tanzania- TANIPAC.

Mkuu wa Wilaya ya Chemba,Simon Chacha akizungumza Wilayani Chemba amesema umuhimu wa chakula unasababisha suala la usalama wa chakula kupewa kipaumbele katika kulinda afya ya jamii na uchumi wa nchi na kuwa kigezo muhimu katika biashara ya kitaifa na kimataifa.

Amesema chakula kisicho salama husababisha madhara ya kiafya na hata vifo kwa walaji pamoja na kusababisha athari za kiuchumi.

“Natambua nafasi yenu kama wafanyabiashara, wasindikaji na wasafirishaji kwa ujumla katika kudhibiti uchafuzi wa sumukuvu kwenye mazao tajwa. Ni kwa mantiki hiyo pia, TBS imeandaa mafunzo haya mahususi kwa ajili yenu ili kuwajengea uwezo juu ya udhibiti wa sumukuvu,”amesema

Amesema, usalama wa chakula unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na uchafuzi wa sumukuvu ambayo husababisha madhara ya kiafya na hata kiuchumi.

“Nimetaarifiwa kuwa pamoja na mada nyingine, kuna baadhi ya mambo muhimu ya kuzingatia yatakayojadiliwa na kutiliwa mkazo na wataalam wakati wa mafunzo.

“Mambo hayo ni pamoja na Kuzingatia kanuni bora za kilimo kama inavyoshauriwa na wataalamu wa kilimo;Kuvuna na kuondoa mahindi na karanga shambani mara tu baada ya kukomaa vizuri; Kukausha vizuri mazao yaliyovunwa kabla ya kuhifadhi.

“Kuhifadhi vizuri mazao na kuepuka wadudu waharibifu, wanyama, joto kali na unyevu; na Kuchambua mahindi na karanga Kabla ya kuhifadhi,”amesema

Pia,amewasihi watalaamu wa afya, lishe, kilimo, mifugo, biashara na maendeleo ya jamii kutoka katika Halmashauri ya Wilaya ya Chemba kuendelea kutilia mkazo na kutoa kipaumbele katika kutekeleza mikakati ya kuimarisha usalama wa chakula ikiwa ni pamoja na kudhibiti uchafuzi wa sumukuvu.

”Hili linawezekana iwapo kutakuwa na ufuatiliaji wa shughuli zinazofanywa na wafanyabiashara wetu,”alisema.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Babati Jocob Lazaro akizungumza Wilayani Babati katika mafunzo kama hayo wamewasihi watalaamu wa afya, lishe, kilimo, mifugo, biashara na maendeleo ya jamii kutoka katika Halmashauri ya Wilaya ya Babati kuendelea kutilia mkazo katika masuala ya chakula.

Amesema pia wanatakiwa kutoa kipaumbele katika kutekeleza mikakati ya kuimarisha usalama wa chakula ikiwa ni pamoja na kudhibiti uchafuzi wa sumukuvu.

”Hili linawezekana iwapo kutakuwa na ufuatiliaji wa shughuli zinazofanywa na wafanyabiashara wetu,”amesema.

Post a Comment

0 Comments