Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI YAMPONGEZA DK. RWEIKIZA KUWEKEZA KWENYE ELIMU

Ofisa Elimu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abdul Maulid, akimkabidhi cheti mmoja wa wahitimu wa darasa la saba, Fatma Mohamed wakati wa mahafali ya 19 ya shule ya St Anne Marie Academy yaliyofanyika shuleni hapo Mbezi Kimara mwishoni mwa wiki. Ofisa Elimu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abdul Maulid, akimkabidhi cheti mmoja wa wahitimu wa darasa la saba, Fatma Mohamed wakati wa mahafali ya 19 ya shule ya St Anne Marie Academy yaliyofanyika shuleni hapo Mbezi Kimara mwishoni mwa wiki. Wanafunzi wa St Anne Marie Academy ya Mbezi Kimara kwa Msuguri wakisrebuka wakati wa mahafali yao ya darasa la saba mwishoni mwa wiki Mkurugenzi wa shule ya St Anne Marie Academy, Dk. Jasson Rweikiza akizungumza wakati wa mahafali ya 19 shuleni hapo mwishoni mwa wiki.

**************************

Na Mwandishi Wetu

SERIKALI imepongeza ubora wa elimu wa shule ya St Anne Marie Academy huku ikizitaka shule zingine kwenda kujifunza mafanikio yake.

Shule hiyo iliyoko Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam inamilikiwa na Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dk. Jasson Rweikiza.

Pongezi hizo zilitolewa mwishoni mwa wiki na Ofisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam, Abdul Maulid, wakati wa mahafali ya darasa la saba ya shule ya St Anne Marie Academy ambapo jumla ya wahitimu 230 walitunukiwa vyeti.

Maulid alisema amefurahishwa na ubora wa elimu unaotolewa na shule hiyo ambayo imekuwa ikiongoza Mkoa wa Dar es Salaam na Wilaya ya Ubungo na kuingia kwenye kumi bora kitaifa mara kwa mara.

“Kuna usemi kwamba usione vyaelea vimeumbwa maana umahiri wa wanafunzi niliouona hapa leo ni jitihada za walimu na menejimenti ya shule nawapongeza sana, shule ziko nyingi sana ila nimeamua kuja hapa St Anne Marie kwasababu hakuna longo longo hapa” alisema

“Mimi ni Ofisa Elimu wa Mkoa mkuu wangu wa mkoa anajua leo St Anne Marie kunanini ameniambia nije hapa na pia kuna Mkurugenzi wa Halmashauri kuna Ofisa Elimu wa Wilaya hapa, mheshimiwa diwani naye yupo hapa, kwanini, wazazi mmechagua shule bora na hamjakosea kuwaleta watoto wenu hapa,” alisema

Aliwataka wazazi kuwalinda watoto dhidi ya ukatili na wasimwamini mtu kuhusu ulinzi wa watoto wao kwani vitendo vya ukatili dhidi yao umekuwa mkubwa sana.

“Watoto hawa ndiyo tunawategemea wapatikane akina Rweikiza, akina Maulid mama Samia, hivyo tusiwachezee watoto hawa, mwanajamii ukiiona mtoto anafanyiwa ukatili toeni taarifa, shule zifanye kama St Anne Marie ziajiri wasimamizi wenye weledi wa hali ya juu,” alisema.

Pia aliwataka wamiliki wa shule wahakikishe mabasi yanayobeba wanafunzi yanakuwa salama kwa wanafunzi na aliwataka wapeleke mabasi hayo yakakaguliwe.

Aliwataka wamiliki wa shule kuacha kuwarundika wanafunzi kwenye basi moja na badala yake wanunue mabasi mengi ili wanafunzi wasibanane kupita kiasi.

“Hata wadhibiti ubora uliowaajiri ndio wamesababisha matokeo mazuri hapa shuleni kwenu ndiyo maana nawataka wengine waje wajifunze St Anne Marie maana haya matokeo hayajaja kutoka hewani tu,” alisema

Alitoa wito kwa shule kuacha kuwachuja wanafunzi kwa kisingizio kwamba wamefanya vibaya kwenye masomo hali ambayo inawapa msongo wa mawazo wazazi.

Aliwataka wamiliki wa shule zote kuhakikisha hawawazuii kufanya mitihani ya mwisho kwa kisingizio kwamba hawajalipa ada kwani sheria na sera ya elimu hairuhusu.

Aliwapongeza wazazi kwa kuendelea kuwasomesha watoto wao akisema kuwa hakuna urithi mzuri kama elimu kwani ni hazina anayoishi nayo miaka yote.

Mkuu wa shule hiyo, Gladius Ndyetabura, alisema matarajio yao ni kuendelea kuwa kwenye 10 bora kitaifa na kuendelea kuongoza Mkoa wa Dar es Salaam na Wilaya ya Ubungo katika matokeo ya kitaifa.

Post a Comment

0 Comments