Ticker

6/recent/ticker-posts

TANZANIA, INDIA KUIMARISHA SEKTA YA UCHUMI

Tanzania na India zimekubaliana kuongeza ushirikiano katika sekta ya uchumi hususan kuendeleza miradi ya maendeleo ya kiuchumi, kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo pamoja na ujenzi wa viwanda.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine alipokutana kwa Mazungumzo na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam

“Tumekubaliana kuwa ni wakati muafaka wa kuongeza ushirikiano wa kiuchumi, hasa kwa kuwa na miradi ya ushirikiano wa sekta ya umma na sekta binafsi (PPP), kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo kuwa na viwanda vitakavyojengwa nchini na kuanza kuzalisha bidhaa mbalimbali ambazo awali zilikuwa zinapatikana nchini India,” amesema Balozi Sokoine.

Viongozi hao pia wamejadili namna ya kuwekeza katika maeneo maalumu ya kibiashara ambapo kutakuwa na uzalishaji wa bidhaa kwa masoko ya nje na ya ndani na kuendeleza falsafa ya Tanzania ya Viwanda.

“Tanzania inamakubaliano na India ya kushirikiana katika masuala ya teknolojia hususan Tehama ambapo hadi sasa India imekubali kuanzisha tawi la Taasisi ya Tehama nchini Tanzania na taasisi hiyo inategemewa kuanza kutoa mafunzo mwakani, ameongeza Balozi Sokoine.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi amesema wamekubaliana namna ya kushirikiana na kuimarisha sekta ya uchumi hususan biashara na uwekezaji kwa maslahi ya pande zote mbili.

Serikali ya India inaamini kuwa Tanzania inaweza kuisaidia katika uwekezaji wa viwanda vikubwa zaidi lakini pia kwa kuwekeza Tanzania, ni rahisi ya kulifikia soko la Jumuiya ya Afrika Mashariki…….“tunataka kuwaleta wawekezaji kutoka India na kuja kuwekeza katika viwanda vya dawa na vifaa tiba hapa Tanzania,” amesema Mhe. Ravi

Mhe. Ravi ameongeza kuwa endapo Serikali ya Tanzania itawapatia eneo maalumu la biashara (Special Economic Zone) la uwekezaji ambalo litasaidia kushawishi wawekezaji kutoka India kuja kuwekeza nchini.

Mwezi Agosti, 2022, Tanzania na India ziliahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano ikiwemo kuhakikisha sekta za afya na nyingine zinaimarika ikiwemo kilimo.


Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi akizungumza na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine akimueleza jambo Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi leo katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Mazungumzo baina ya Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine katika picha ya pamoja na Ujumbe wa India unaoongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje India, Mhe. Dammu Ravi katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam


Post a Comment

0 Comments