Ticker

6/recent/ticker-posts

ORYX ENERGIES YAKABIDHI MITUNGI YA GESI KWA WANAWAKE WAJAWAZITO WILAYANI SERENGETI, VIONGOZI WAPONGEZA


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mary Masanja (watatu kulia) akipokea mtungi wa gesi kutoka kwa Meneja Masoko wa Kampuni ya Oryx Peter Ndomba(wan ne kushoto).Tukio hilo limefanyika jana eneo la Rubanda wilayani Serengeti mkoani Mara wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti iliyoratibiwa na Taasisi ya Doris Mollel Foundation ambayo imejikita katika kusaidia mtoto njiti na lengo la mitungi hiyo ni kuwawezesha wanawake kutumia nishati safi ya kupikia.

Meneja Masoko wa Kampuni ya Oryx Peter Ndomba (wa tatu kulia) akikabidhi mtungi wa gesi kwa mmoja ya wanawake wajazito wa Kata ya Rubanda kwa niaba ya wanawake wengine wajawazito wa wilaya ya Serengeti.Wa pili kulia ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mary Masanja akishuhudia utolewaji wa mitungi hiyo ya gesi kwa wanawake wajawazito wa Wilaya ya Serengeti mkoani Mara.


Meneja Masoko wa Kampuni Peter Ndomba(kulia) akipokea cheti cha shukrani kutoka kwa Naibu Waziri wa Afya Dk.Godwin Mollel wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti.Cheti hicho kimeandaliwa na Taasisi ya Doris Mollel Foundation ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa wadau hao katka kusaidia taasisi hiyo.

Naibu Waziri wa Afya Dk.Godwin Mollel (kushoto) akizungumza umuhimu wa kutumia nishati safi ya kupikia baada ya Kampuni ya ORYX Energies kukabidhi mitungi ya gesi na majiko yake kwa wanawake wajawazito wilayani Serengeti kupitia Taasisi ya Doris Mollel Foundation.

Doris Mollel ambaye ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Doris Mollel Foundation akisoma jina la mmoja ya wadau walioshiriki kufanikisha Siku ya Mtoto Njiti Duniani wakati wa maadhimisho ya siku hiyo yaliyofanyika wilayani Serengeti mkoani Mara.

***********************

Na Mwandishi Wetu, Serengeti

KAMPUNI ya Oryx Energies imekabidhi mitungi ya gesi 200 pamoja na majiko yake kwa kwa Taasisi ya Doris Mollel Foundation inayojishughulisha kusaidia watoto njiti pamoja na malezi ya watoto hao ambapo mitungi hiyo imetolewa kwa wanawake wajawazito katika Wilaya ya Serengeti mkoani Mara kuwaondolea adha ya kutafuta kuni kwa ajili ya kupikia.

Mitungi hiyo ya gesi ikiwa na majiko yake imekabidhiwa leo Novemba 20 mwaka 2022 kwenye Maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti Duniani ilyofanyika Kata Rubanda wilayani Serengeti mkoani Mara na kuhudhuriwa na wananchi pamoja na viongozi wa Serikali akiwemo Naibu Waziri wa Afya Dk.Godwin Mollel, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mary Masanja, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani.

Uamuzi wa kampuni hiyo kutoa mitungi hiyo umepongezwa na viongozi mbalimbali walioshiriki maadhimisho hayo ambao wameeleza kitendo cha mama mjamzito kupewa mtungi wa gesi na jiko lake inakwenda kutoa nafasi mama kulea familia na hasa watoto na kuondokana na adha ya kwenda kukata kuni kwa ajili ya kupikia.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Marry Masanja amesema Oryx imeona umuhimu wa kushiriki katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti kwa kutoa mitungii ya gesi na hiyo inakwenda kusaidia kutunza mazingira na wamekuwa mfano wa kuigwa kwani ndio kampuni ya mwanzo kabisa kuja na nishati safi ya kupikia.

“Tunawapongeza kwa jitihada zao za kuhakikisha jamii yetu inakuwa na nishati safi ya kupikia ambayo pia inasaidia katika kutunza mazingira.Kutumia nishati safi ya kupikia inasaidia katika jitihada za Wizara ya Maliasili na Utaliii kulinda na kutunza mazingira, takwimu zinaonesha asilimia 90 ya nishati isiyo safi yaani mkaa na kuni ndio inayotumika kwenye kupikia,”amesema.

Aidha ametoa ombi kwa wadau wanaohusika na kampuni za nishati safi za kupikia kuangalia namna ya kuifanya nishati hiyo kupatikana kwa bei nafuu ambayo kila mwananchi anaweza kumudu kununua jiko la gesi.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya Dk .Godwin Mollel pamoja na kuzungumzia hatua zinazochukuliwa na Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuboresha afya ya mama na mtoto ikiwemo afya ya Mtoto Njiti pia anatoa pongezi kwa Taasisi ya Doriss Mollel katika kuokoa maisha ya Watoto Njiti na kuendelea kutoa kila aina ya misaada inayogusa jamii ya watoto njiti.

"Rais siku zote amekuwa akionesha njia lakini kwenye vifo vya mama na mtoto ni eneo ambalo linamgusa sana .Hata kwenye hotuba yake ya kwanza bungeni alionesha msisitizo mkubwa.Katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti Duniani Rais wetu ameweka fedha kwenye akaunti ya Doris Mollel Foundation Sh.milioni 20.Pia Rais ametoa Sh.milioni 50 kwa ajili ya kununuliwa vifaa kwa ajili ya Watoto Njiti.Kupitia bajeti ya mwaka huu Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kujengwa vituo 100 vitakavyohusika na matibabu ya watoto njiti.

"Aidha nampongeza Dorris Mollel kwa mchango wake wa kusaidia jamii hasa watoto njiti, amekuwa hafanyi semina wala makongamano lakini kila anapoonekana anagusa jamii moja moja.Lakini leo hapa tumeshuhudia mitungi ya gesi 200 inakabidhiwa kwa wamama wajawazito."Nishati safi ya kupikia inakwenda kupunguza uharibifu wa mazingira na tunafahamu mabadiliko ya kimazingira yanachangia uwepo wa Watoto njiti.”

Awali Meneja Masoko wa Kampuni ya ORYX Energies Peter Ndomba aliyemwakilisha Mkurugenzi wa kampuni hiyo, amesema wao wameamua kuonesha njia kwa kuamua kutoa mitungi ya gesi kwa ajili ya kumuwezesha wamama wajawazito kuwa na nishati safi ya kupikia.

“Tangu tulipoingia Tanzania mwaka 1999 moja ya ajenda yetu kuu ni kutetea mazingira kwa kuhakikisha jamii inakuwa na nishati safi ya kupikia lakini pili kuimarisha afya ya watanzania hususani ya Mama ambaye amekuwa mstari wa mbele katika familia kwa upande wa mapishi , na Doris Mollel Foundatuion alipotuomba mitungi ya gesi hatukusita kumpatia kwasababu sisi tulimuona mama moja kwa moja., hivyo tuliamua kushiriki bila kusita.

Aidha amesema mitungi ambayo wameitoa kwa wanawake wajawazito ni sehemu ya kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan inayohamasisha Watanzania kutumia zaidi nishati safi ya kupikia badala ya kuendelea kukata kuni ambayo imekuwa ikichangia kuharibu mazingira.

Kwa upande wake wa Doris Mollel ambaye ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Dorris Mollel Foundation ameishukuru kampuni ya ORYX kwa kumpatia mitungi hiyo ambayo aliiomba kwa ajili ya kuwasaidia wanawake wajawazito ambao ndio wamekuwa wakihangaika kutafuta kuni kwa ajili ya kupikia, hivyo kupatikana kwa mitungi hiyo kunakwenda kumuondolea mama mjazito changamoto ya kutafuta kuni.

“Wakati wa mjadala wa nishati safi ya kupikia ambao ulihudhuriwa na Rais Samia Suluhu Hassan , ndo siku ambayo nilikutana na Mkurugenzi wa Oryx ambaye alishiriki mjadala huo na hivyo nilitumia nafasi hiyo kumuomba mitungi ya gesi na majiko yake ili nikawapatie wanawake wajawazito.Nashukuru leo nakabidhi mitungi hii na ndoto yangu imetimia ya kuona tunatafuta ufumbuzi wa kumuondolea adha mama mjamzito ya kwenda mbali kutafuta kuni.”

Aidha ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wadau wengine waljochangia vifaa mbalimbali kwa ajili ya kusaidia watoto njiti lakini kwa upekee anatoa shukrani kwa Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amempatia Sh.milioni 20 kufanikisha maadhimisho hayo pamoja na Sh.milioni 50 kwa ajili ya kununua vifaa mbalimbali kwa ajili ya kusaidia Mtoto Njiti.

Post a Comment

0 Comments