Ticker

6/recent/ticker-posts

BARRICK YAAHIDI DOLA MILIONI 30 ZA MAENDELEO YA SHULE KWA UBIA NA TANZANIA


 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea mfano wa hundi yenye thamani ya Dola za Marekani (USD) 30,000,000.00 kutoka kwa Mtendaji Mkuu ambaye pia ni Rais wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Mark Briston kwa ajili ya shughuli mbalimbali za Elimu, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 20 Machi, 2023. Fedha hizo zitatumika katika ujenzi wa Mabweni 273 pamoja na Madarasa zaidi ya 1094 kwa Wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Mtendaji Mkuu ambaye pia ni Rais wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Mark Briston, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 20 Machi, 2023.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa katika picha ya pamoja na Mtendaji Mkuu ambaye pia ni Rais wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation Mark Briston mara baada ya mazungumzo Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 20 Machi, 2023.


Dodoma, Tanzania, Machi 20, 2023 – Kampuni ya Dhahabu ya Barrick (NYSE:GOLD) (TSX:ABX) - Katika mkutano wa leo kati ya rais na afisa mtendaji mkuu wa Barrick, Mark Bristow na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kampuni hiyo ilithibitisha ahadi yake ya Dola Milioni 30 (takriban shilingi bilioni 70.5 za fedha za Tanzania) kwa ajili ya upanuzi wa miundombinu ya elimu nchini Tanzania kwa ushirikiano na Serikali.


Programu ya Barick-Twiga ya Kusongesha Mbele Mustakabali wa Elimu, iitwayo “Barrick-Twiga Future Forward Education Program” inalenga kujenga madarasa 1,090, majengo ya maliwato na vyoo 1,640 na mabweni 270 katika shule 161 nchini kote ili kusaidia kuwapatia malazi wanafunzi takribani 49,000 kati ya wanafunzi wapatao 190,000 wanaotarajiwa kuanza masomo yao ya sekondari ya juu (A-level) Julai mwaka huu. Dola milioni 10 za kwanza zitalipwa mwezi Aprili na albaki itatolewa kadiri programu hiyo itakavyokuwa inaendelea.


“Tunaamini kuwa elimu ni muhimu kwa maendeleo ya nchi. Migodi yote miwili ya dhahabu ya Bulyanhulu na North Mara inaendelea kusaidia sekta ya elimu kwa kujenga vyumba vya madarasa na kuboresha miundombinu ya elimu katika maeneo yanayoizunguka migodi hiyo, jambo ambalo limefanikisha baadhi ya shule hizo kuwa miongoni mwa shule zinazoongoza mara kwa mara katika mikoa hii,”
alisema Bristow.


North Mara tayari imetumia dola milioni 1.9 (shilingi bilioni 4.5) katika shule 87 za msingi na sekondari wilayani Tarime, shule 14 kati ya hizo zikiwa zile zilizofanya vizuri zaidi wilayani humo. Bulyanhulu imetumia dola milioni 1.8 (shilingi bilioni 4.2) katika miradi 80 ya elimu katika eneo linalouzunguka mgodi huo na hivi sasa inajenga Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi katika Kijiji cha Bunango. Uwekezaji wa Barrick katika eneo linalouzunguka mgodi huo umewezesha wasichana wa Kitanzania 7,557 kupata elimu mwaka 2022.


“Licha ya msaada wa kampuni wa kustawisha elimu, mwaka jana, North Mara ilitambuliwa rasmi kama mlipakodi mkubwa zaidi nchini Tanzania na Bulyanhulu ilitunukiwa Tuzo ya Mwajiri Bora anayezingatia matakwa ya sheria, ambayo ilitolewa na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii. North Mara na Bulyanhulu pia zilipata tuzo za mshindi wa kwanza na wa pili, mtawalia, kwa uuzaji wa madini nje ya nchi na kwa kuingiza fedha za kigeni nchini. Kampuni zote mbili zimetoka mbali sana na tunatarajia kuendelea na safari hiyo kupitia ubia wetu wa Twiga na serikali.”


Bristow alisema tangu Barrick ilipoichukua migodi hiyo mwaka 2019, imeingiza dola bilioni 2.4 katika uchumi wa Tanzania. Kupitia kamati zake za maendeleo ya jamii, migodi hiyo imewekeza zaidi ya dola milioni 10 katika miradi ya kuboresha huduma za afya, elimu, upatikanaji wa maji ya bomba na miundombinu ya barabara.

 

Kwa maelezo zaidi kutoka Barrick

Meneja wa nchi wa Mawasiliano na uhusiano

wa Kampuni

Georgia Mutagahywa

+255 754 711 215

Baruapepe: georgia.mutagahywa@barrick.com

Mahusiano ya Kampuni na wawekezaji na vyombo vya habari

Kathy du Plessis

+44 20 7557 7738

+27 83 266 5847

Baruapepe: barrick@dpapr.com

Tovuti: www.barrick.com



Post a Comment

0 Comments