Ticker

6/recent/ticker-posts

RAIS SAMIA AMEDHAMIRIA KUWAINUA VIJANA WENYE ULEMAVU – KATAMBI


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi (kulia) akizungumza na mnufaika wa mafunzo ya ufundi stadi mwenye Ulemavu, Bw. Benjamin Benjamin alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari, mkoani Tabora kwa lengo la kukagua maendeleo ya mafunzo hayo.


Kijana mwenye Ulemavu mnufaika wa mafunzo ya ufundi stadi, Bw. Dotto Lukuni (kulia) akieleza namna walivyoshona shati kwa ajili ya Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari.


Kijana mwenye Ulemavu mnufaika wa mafunzo ya ufundi stadi, Bw. Samwel Shaban (kushoto) akifafanua jambo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari katika darasa la fani ya ufundi umeme.


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi akijaribu shati ya kitenge aliyoshonewa na vijana wenye Ulemavu wanufaika wa mafunzo ya ufundi stadi mwenye Ulemavu, Bw. Benjamin Benjamin alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari, mkoani Tabora kwa lengo la kukagua maendeleo ya mafunzo hayo.


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi akiangalia kitabu cha nukta nundu kwa ajili ya wasioona alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari, mkoani Tabora kwa lengo la kukagua maendeleo ya mafunzo yanayotolewa kwa vijana wenye Ulemavu. Wa pili kutoka (kushoto) ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Mhe. Louis Bura.


Sehemu ya vijana wenye Ulemavu fani ya Useremala wakiendelea na mafunzo katika chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari, mkoani Tabora.



PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU

(KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU)

Na: Mwandishi Wetu – TABORA



Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Mhe. Patrobas Katambi amesema Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuhakikisha vijana wenye Ulemavu wanapata ujuzi unaostahili na mitaji ili kujikwamua kiuchumi.



Aidha, amepongeza juhudi na ubunifu wa vijana hao wenye Ulemavu wanaopata mafunzo ya stadi za kazi kwenye Vyuo vya Ufundi Stadi na Marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu vinavyomilikiwa na Serikali kwa kuonesha umahiri katika mafunzo yao.



Amesema hayo wakati wa ziara ya kujionea utekelezaji wa mafunzo hayo alipotembelea chuo cha ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Luanzari, mkoani Tabora.



Naibu Waziri Katambi amesema kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kukuza ustawi kwa Watu wenye Ulemavu nchini sambamba na kuboresha huduma mbalimbali ili kuwezesha kundi hilo kushiriki kikamilifu katika kusukuma gurudumu la maendeleo.



“Katika kipindi cha miaka miwili ya uongozi wa Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kupitia Mpango wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO – 19 alitoa fedha zaidi ya bilioni 3.4 kwa ajili ya ukarabati wa vyuo vinne vya ufundi stadi na marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu. Lengo la Rais Samia ni kuona kundi hilo linawezeshwa kiujuzi na mitaji ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na utegemezi,” amesema



Amebainisha kuwa serikali haitegemei kumuona mtu wenye Ulemavu Tanzania akipata changamoto.



“Vijana hawa wakitoka hapa watakuwa mafundi wabobezi kutokana na ujuzi waliopata na hatuwaachi na ujuzi pekee, tutawawezesha kupata mitaji ya kuanzisha shughuli za uzalishajimali kupitia halmashauri zenu,”



Akiwasilisha taarifa ya chuo hicho pamoja na utekelezaji wa mafunzo hayo, Mkuu wa Chuo cha Ufundi Stadi na Marekebisho kwa Watu wenye Ulemavu Tabaora, Bi. Halima Lugoye ameeleza kuwa uboreshaji wa mazingira ya chuo hicho imekuwa ni chachu ya ongezeko kubwa la vijana kujitokeza kwa wingi kupata ujuzi.

Akitoa neno la shukrani mnufaika wa Mafunzo ya Ujuzi, Joyce Terezu anayesoma fani ya Ushonaji ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutambua mchango walionao vijana wenye Ulemavu katika ujenzi wa Taifa.

“Tunamshukuru Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuwezesha sisi Watu wenye Ulemavu, maana tulikuwa hatuthaminiwi hali iliyosababisha tuwe watu ambao ni tegemezi lakini leo hii Rais Samia ametutoa huko na kutuleta mahali hapa kuja kupata ujuzi wa fani mbalimbali,” amesema Terezu

Post a Comment

0 Comments