Ticker

6/recent/ticker-posts

KIONGOZI WA MBIO ZA MWENGE 2023 AAGIZA KUONDOLEWA KWA VITI NA MEZA MBOVU KATIKA SHULE YA SEKONDARI VITA KAWAWA WILAYANI NAMTUMBO

Kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2023 Abdala Shaibu Kaim,akizungumza na wanafunzi,wazazi na viongozi wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma baada ya kukagua ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa katika shule ya sekondari Rashid Kawawa,kushoto Mkuu wa wilaya hiyo Ngolo Malenya.
Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka 2023 Abdala Shaibu Kaim kulia na mkimbiza Mwenge Kitaifa Michael Mkaga kushoto wakikagua ubora wa viti na meza katika shule ya sekondari Vita Kawawa wilayani Namtumbo ambapo walibaini kuwepo kwa viti zaidi ya 115 vibovu.

Jengo la vyumba vitatu vya madarasa katika shule mpya ya Sekondari Vita Kawawa wilayani Namtumbo vilivyojengwa ili kuwanusuru wanafunzi wanaotoka kata ya kijiji cha Suluti kwenda maeneo mengine kwa ajili ya masomo yao.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023 Abdala Shaibu Kaim kushoto akikagua ubora wa viti na meza zilizowekwa kwenye shule ya Sekondari Vita Kawawa wilayani Namtumbo,kulia Mhandisi wa ujenzi wa Domisian Panga.

*********************

Na Muhidin Amri,
Namtumbo

KIONGOZI wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2023 Abdalla Shaib Kaim,amemwagiza Mkuu wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma Ngolo Malenya kuhakikisha anasimamia zoezi la kuondoa viti na meza katika shule ya Sekondari Vita Kawawa zilizotengenezwa chini ya kiwango.

Sambamba na hilo,ametoa wiki mbili kwa Mhandisi wa ujenzi wa Halmashauri ya wilaya Namtumbo na mafundi waliotengeneza thamani hizo,kutengeza upya viti na meza kwa gharama zao bila kutumika fedha za serikali.

Kiongozi huyo wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2023,amelazimika kutoa maagizo hayo baada ya kutoridhishwa na ubora wa viti na meza hizo zilizowekwa kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi wa shule hiyo.

Aidha amemtaka Mkuu wa Takukuru wilayani humo,kufanya uchunguzi wa Sh.milioni 600 zilizotumika katika ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa baada ya kukosekana kwa baadhi ya nyaraka muhimu za matumizi na ununuzi wa vifaa mbalimbali kwenye ujenzi wa mradi huo.

Alisema ikibainika kuna matumizi mabaya ya fedha hizo, watu wote waliohusika wachukuliwe hatua ikiwemo kuwafikisha mahakamani na kuwataka watumishi wa umma kuwa na uchungu na waadilifu wa mali za serikali katika maeneo yao ya kazi.

“majengo ya shule yamejengwa kwa viwango na ubora wa hali ya juu,lakini asilimia kubwa ya meza na viti ni vibovu,nakuomba Mkuu wa wilaya simamia zoezi la kuondoa viti na meza 115 zenye kasoro na nipate taarifa ndani ya wiki mbili”alisema.

Mkuu wa shule hiyo Efraim Mwale alisema,ujenzi wa mradi wa vyumba vitatu vya madarasa katika shule ya Sekondari Vita Kawawa ulianza mwezi Oktoba na kukamilika mwezi Disemba mwaka 2022.

Alisema,mradi huo umetekelezwa kwa fedha kutoka serikali kuu ambayo imetoa jumla ya Sh.milioni 60,000 na umetekelezwa kwa mfumo wa lipa kwa matokeo(Ep4R).

Mwale alisema,vyumba hivyo ni miongoni mwa vyumba 17 vya madarasa vilivyojengwa katika shule mbalimbali za sekondari katika Halmashauri ya wilaya Namtumbo kwa lengo la kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2023.

Alisema,dhumuni la mradi huo ni kuongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na elimu ya Sekondari ndani ya wilaya na kuondoa msongamano wa wanafunzi katika vyumba vya madarasa.

Alisema,mradi huo unalenga kuwapunguzia umbali wanafunzi wanaotoka kitongoji cha Suluti kwenda kwenye shule Mama ya Nasuli iliyoko kilomita 3.

Post a Comment

0 Comments