Ticker

6/recent/ticker-posts

Maadhimisho ya Siku ya Vipimo Duniani, TBS yanena

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limeungana na mataifa mengine duniani kufanya maadhimisho ya siku ya Vipimo ambayo hufanyika Mei 20 kila mwaka ambapo TBS imeitumia maadhimisho hayo kutoa elimu na hamasa kwa wadau wa vipimo kuhakiki vipimo kwa lengo la kumlinda mtumiaji.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 20,2024 Jijini Dar es Salaam Afisa Metrolojia Mwandamizi TBS, Joseph Kadenge amesema kupitia Kauli Mbiu ya maadhimisho kwa Mwaka huu ni "Tunapima leo kwa kesho endelevu", amewataka wenye viwanda na wadau mbalimbali kutumia huduma za TBS kwa kuhakiki vipimo kwenye sekta mbalimbali ili kupata usahihi wa vipimo hivyo hatimaye kuweza kumlinda mtumiaji.

Kadenge amesema kuwa ni vyema wadau katika sekta mbalimbali wakaendelea kuhakiki vipimo vyao ikiwemo mahospitalini, viwandani, kwenye sekta ya mafuta na gesi na wengineo ili kuwa na vipimo sahihi.

Ameeleza kuwa TBS imeandaa semina kuhusu Siku ya Vipimo Duniani kwa Tanzania ambapo kwa mwaka huu imepangwa kufanyikia mkoani Mbeya ili kutoa uelewa kwa wananchi kuhusu masuala ya Umuhimu wa vipimo.

Kwa upande wake Afisa Vipimo Mkuu Maabara ya Vipimo ya Taifa Metrolojia, Joseph Mahilla amesema maadhimisho hayo yanafanyika kila mwaka na TBS huhakikisha elimu ya vipimo inawafikia wadau wote wa vipimo nchini

Amesema Shirika la Viwango linashughulika na Vipimo viwili vya metrolojia ambayo ya kwanza ni Sayansi ya Vipimo msingi ambayo inajihusisha zaidi na tafiti na sehemu ya pili ni Sayansi ya Vipimo viwandani .

Pamoja na hayo amebainisha kwamba TBS ina maabara ya kisasa ya vipimo na yenye umahiri hivyo ni vyema wadau kuendelea kuitumia kwa manufaa na maendeleo ya viwanda

Post a Comment

0 Comments