Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI MKUU AMPONGEZA PROF. SHEMDOE KWA UTENDAJI KAZI MBELE YA WANANCHI

   

Na OWM - TAMISEMI, Lushoto

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba amesifu utendaji kazi wa Mbunge wa Lushoto ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu -TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe kwa namna anavyotumia uzoefu wake wa utendaji kazi Serikalini katika kuwahudumia na kuwaletea maendeleo wananchi wa Lushoto, ikiwa ni pamoja na kutekeleza jukumu la kusimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Dkt. Nchemba amempatia maua yake Prof. Shemdoe Februari 17, 2026 mbele ya wananchi wa Lushuto alipozungumza nao, mara baada ya kuzindua rasmi mtambo wa kuzalisha hewa tiba ya oksijeni katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto. 

“Nikiri mna Mbunge makini, mwenye hadhi, mzoefu wa utendaji kazi Serikalini, ameshaitumikia Serikali katika nyadhifa mbalimbali kwenye wizara kadhaa hivyo anafahamu jambo lolote linalohusu maendeleo ya Lushoto lishughulikiwaje na ni wizara ipi itahusika,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Mhe. Waziri Mkuu  amewaeleza wananchi wa Lushuto kuwa wamepata kiongozi jembe na mchapa kazi ambaye yuko tayari kuwaletea maendeleo wana Lushoto hivyo wamuunge mkono ili aweze kutimiza ndoto yake ya kuwatumikia wananchi wa Jimbo la lushoto.

Aidha, Dkt. Nchemba amemtaka Mwenyekiti wa Halmashauri na Madiwani kumsaidia Prof. Shemdoe kwa kuwatembelea wananchi, kusikiliza kero zao na kuziwasilisha kwa Prof. Shemdoe ili aweze kuzifanyia kazi kwani kutokana na majukumu ya kitaifa aliyonayo Prof. Shemdoe kuna wakati anakosa muda wa kuwatembelea wananchi na kupokea simu zao mara kwa mara.

“Kutokana na majukumu aliyonayo Prof. Shemdoe anapaswa kushughulika na mambo makubwa ya kimaendeleo kwa kuhakikisha fedha za utekelezaji zinafika kwa wakati, hivyo Mwenyekiti wa Halmashauri na Madiwani mkutane na wananchi na muwasilishe changamoto za wananchi hao kwa Prof. Shemdoe ili azifanyie kazi,” ameelekeza Dkt.  Nchemba. 

Dkt. Mwigulu Nchemba amewaeleza wananchi wa jimbo la Lushoto kuwa kitendo cha Prof. Shemdoe kuaminiwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na kumpatia dhamana ya kusimamia Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa wasitarajie atafanya ziara za kutembelea vitongoji kila mara na badala yake ziara hizo zitafanywa na madiwani.

Post a Comment

0 Comments