Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI MKUU: ANZISHENI MAJUKWAA YA KIUCHUMI

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na watumishi wa Ubalozi wa Tanzania Afrika Kusini alipoutembelea Ubalozi huo ulioko jijini Pretoria, Kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi na wa pili kulia ni Kaimu Balozi wa Afrika Kusini Balozi, Peter Shija (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Ubalozi wa Tanzania Afrika Kusini alipoutembelea Ubalozi huo ulioko jijini Pretoria Ijumaa Desemba 30, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na watumishi wa Ubalozi wa Tanzania Afrika Kusini alipoutembelea Ubalozi huo ulioko jijini Pretoria, Desemba 30, 2022. wa kwanza kulia ni Kaimu Balozi wa Afrika Kusini Balozi, Peter Shija (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

*********************


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameagiza viongozi na watumishi katika balozi waendelee kufanya tathmini ya fursa za kiuchumi ambazo Tanzania inaweza kupata kutokana na ushirikiano wa kidiplomasia kwenye nchi walizopo.

Amesema ni vema balozi hizo zikaanzisha majukwaa ya kiuchumi yatakayowakutanisha wafanyabiashara na wawekezaji wa nchi hizo katika sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwemo ardhi, madini, utalii, mawasiliano na biashara.

“Muwasihi wafanyabiashara na wawekezaji waje kuwekeza Tanzania na washirikiane na Watanzania kufungua makampuni, hii itatusaidia Watanzania kubadilishana uzoefu wa namna bora ya kuendesha biashara.”

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Ijumaa, Desemba 30, 2022) wakati akizungumza na watumishi wa ubalozi wa Tanzania ulioko jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Amesema watumishi wa balozi za Tanzania hawana budi kuandaa makubaliano baina ya Tanzania na nchi walizoko ambayo yataonesha nini kinatakiwa nchini humo na ambacho kinapatikana kwa wingi nyumbani Tanzania.

“Hapa kwenu, ubalozi unapaswa kutengeneza makubaliano maalum ya kibiashara miongoni mwa nchi hizi mbili na kubainisha aina ya bidhaa ambazo zinapatikana Tanzania kwa wingi na zinahitajika Afrika Kusini,” amesisitiza.

Aidha, Waziri Mkuu amesema ni vema pia ubalozi huo ukaendelea kuhamasisha watalii kutoka nchini humo kwa kubainisha vivituo vya utalii vilivyoko Tanzania ambavyo nchi hiyo haina huku akitolea mfano Mlima Kilimanjaro.

Awali, akitoa taarifa ya kiutendaji ya ubalozi huo, Kaimu Balozi Peter Shija alisema Tanzania inaweza kunufaika zaidi na fursa za biashara zilizopo nchini humo kwa kuuza mazao kama, mchele, maharage, korosho na mazao ya matunda.

Post a Comment

0 Comments