Ticker

6/recent/ticker-posts

COSTECH KUENDELEA KUSIMAMIA MIRADI INAYOENDELEA 2023/24

Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia COSTECH katika kipindi cha mwaka wa fedha 2023/24 imesema inaendelea kusimamia miradi inayoendelea ukiwemo wa Kigoda cha Utafiti katika Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) na Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) ambao ni mradi wa miaka mitano, wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 5 pamoja na kushirikiana na Mabaraza ya Kikanda na Kimataifa kuhakikisha tunashiriki kutafuta fursa ambazo zitaendelea kuleta fedha za utafiti kupitia COSTECH au kuhamasisha Taasisi za ndani kuomba hizo fursa,

Hayo yamesemwa leo jijini Dodoma katika ukumbi wa Habari Maelezo na Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH Dkt. Amos Nungu alipokuwa akiongea na waandishi wa Habari mafanikio ya COSTECH kwa mwaka 2022/23 na mwelekeo wa vipaumbele vya taasisi kwa mwaka wa fedha 2023/24.

Dkt. Nungu pia ameelezea pia ukamilishaji wa zoezi la ufadhili wa pamoja wa miradi ya utafiti wa Mabaraza ya Utafiti duniani ikiwa ni njia mojawapo ya kuongeza kuonekana kwa watafiti wetu na kuitangaza nchi yetu katika nyanja hii ya utafiti pamoja na kukamilisha mchakato na kutoa fedha kwa maandiko mawili kwa kutoa mrejesho kwa walioshiriki lakini wakakosa, na kuwatembelea walioshinda.

Vilevile, Dkt. Nungu amesema kupitia mradi wa HEET, COSTECH imeboresha mifumo mbalimbali ili kuongeza ufanisi zaidi katika suala la uratibu wa Tume. Ikumbukwe kuwa mradi huu ni mahususi kwa Taasisi za Elimu ya Juu hivyo, inabidi tuwe tayari kuwahudumia baada ya kukamilisha mabadiliko wanayofanya kupitia mradi huo.

Aidha kwa upande wa ubunifu Dkt. Nungu amesema COSTECH itakamilisha karakana ya mbunifu wa prepaid water meter iliyopo SIDO Vingunguti ili kuzalisha mita kwa wingi na kwa wakati kukamilisha ufungaji wa mita hizo za maji kwa mikoa 15 iliyobaki, lakini pia kusimamia Kongano Bunifu mpya ikiwemo ya Mafia (nazi) Geita (uchimbaji dhahabu) na Kigoma (mawese) na kufanya kazi na kumbi za Bunifu na wadau wengine kuhakikisha mazingira wezeshi yanaimalika zaidi.

Katika kuratibu Utafiti na Ubunifu, COSTECH inaendelea kufanya kazi na wadau mbalimbali, kubwa ni kufanikisha kuweka mazingira wezeshi ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa rasilimali fedha, sera na miongozo stahiki, mashirikiano, miundombinu, nk. ili kuhakikisha mchango wa utafiti na ubunifu unaleta manufaa kwa taifa.

Post a Comment

0 Comments